0

TAZAMA VIDEO HII TAMU YA AINA YAKE HAPA CHINI


Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ipo na inaendelea kuwatumikia wananchi wake kama kawaida.


Dk. Shein alisema hayo alipokuwa katika ziara ya kukagua mradi wa uimarishaji huduma ya maji safi na salama Makunduchi, mkoa wa Kusini Unguja jana, akiwa ameambatana na viongozi waandamizi wa serikali yake.

“Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ipo na inaendelea na kazi zakuwahudumia wananchi wake kama kawaida,” alisema Rais Dk. Shein na kuongeza:

“Serikali itaendelea kuimarisha upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi katika maeneo yenye upungufu wa huduma hiyo.”

Mradi huo umehusisha ujenzi wa tangi pamoja na uchimbaji wa kisima ili kuondoa tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama kwa wakazi wa Makunduchi.

Alisema SMZ itaendelea kuwahudumia wananchi wote na hatua ya kukamilika kwa mradi huo ni faraja kwa serikali na wananchi wake.

Rais huyo wa Zanzibar alisema mradi huo unaotarajiwa kuzinduliwa katika sherehe za Mapinduzi, utaongeza upatikanaji wa maji safi na salama na kumaliza kero ya maji kwa wananchi.

Dk. Shein alisema visima vitatu vilivyochimbwa vitapeleka maji katika tangi kubwa linalotarajiwa ujenzi wake kukamilika ndani ya wiki moja kwa ufadhili wa taasisi ya Ras el Khaimah visiwani humo.

Aidha, Dk. Shein aliwapongeza wafanyakazi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (Zawa) na uongozi wa Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji na Nishati, kwa kufanikisha mradi huo muhimu.

Kwa upande wake, Waziri wa Ardhi, Makazi, Maji na Nishati, Ramadhan Abdallah Shaaban, alisema si muda mrefu wananchi wa maeneo hayo watafaidika na mradi huo wa maji safi na salama baada ya kukamilika.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Zawa, Dk. Mustafa Ali Garu, alisema visima hivyo vitatu vitakapokamilika vitatoa huduma ya maji safi na salama kwa asilimia zaidi ya 90 kwa wananchi wa Makunduchi.

Post a Comment

WRITE YOUR COMMENTS HERE

 
Top